
Na Nyangusi Ole Sang’ida
Tarehe 17 Aprili 2025, Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mhe. Festo Kiswaga, alifanya ziara ya kikazi katika kata ya Mswakini ili kusikiliza kero za wananchi na kushughulikia changamoto za ardhi. Katika ziara hiyo, Mhe. Kiswaga aliwahakikishia wakazi wa Mswakini kuwa ardhi yao ya malisho italindwa kwa manufaa ya vizazi vijavyo, akisisitiza umuhimu wa kulinda rasilimali za jamii.
Mhe. Kiswaga aliwaasa wananchi kuvutia wawekezaji wa utalii, akibainisha kuwa eneo la Mswakini, lililo karibu na hifadhi ya wanyama na Ziwa, lina uwezo mkubwa wa kiuchumi. “yaani ninyi mpo katikati ya pesa,fanyeni hivyo ili mumsaidie Rais kuongeza idadi ya watalii” alisema. Aidha, aliwataka wakazi wasikae kimya wanaposhuhudia vitendo vya kuuza ardhi bila ridhaa yao, akisema, “Pigeni kelele..Tumieni huu ushauri mtakuja kunishukuru.”
Katika hatua ya maana, Mhe. Kiswaga alifanikisha kumaliza mgogoro wa ardhi uliokuwa unatishia amani Mswakini. Tume iliyoundwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ilichunguza suala hilo na kutoa mapendekezo yaliyosababisha kurejeshwa kwa eneo la malisho lililovamiwa. “Eneo lililozidi lizrudi kwenye serikali ya kijiji,” alisema Kiswaga.
Ziara hii inaonyesha dhamira ya Mhe. Kiswaga ya kuhakikisha haki za wananchi wa Monduli zinazingatiwa, hasa katika masuala ya ardhi. Kwa wale wanaotaka kufuatilia masuala ya ardhi na maendeleo Monduli, endelea kushikamana nasi kwa habari zaidi.