
Aliamka asubuhi akiwa na maumivu ya kichwa, Akaenda duka la dawa, akaeleza dalili, na kupewa dawa. Bila vipimo, bila ushauri wa daktari,Siku mbili baadaye hali yake ikawa mbaya zaidi. Hii si hadithi tu ila hii ni hali halisi ya maelfu ya Watanzania.
Bi. Fatuma Yusuph ni mmoja wa mashuhuda wa hatari ya matumizi ya dawa kiholela. “Nilijua ni malaria, nikameza dawa… kumbe haikuwa hivyo, Nilizidiwa,” anasema Fatuma.
Wataalamu wa afya wanazidi kutoa tahadhari, Mfamasia John Kazitanga anasema, “Dawa si kitu cha kufikiria kirahisi, lazima historia ya mgonjwa, dalili, na vipimo vijulikane” Vinginevyo, kinachodhaniwa kuwa tiba, kinaweza kuwa sumu.

Kwa mujibu wa utafiti wa Wizara ya Afya wa mwaka 2022, asilimia 59.8 ya Watanzania yaani takriban watu 6 kati ya kila 10 wanatumia dawa bila ushauri wa wataalamu. WHO inaongeza kuwa watu 700,000 hufariki kila mwaka duniani kutokana na usugu wa dawa – hali inayosababishwa kwa kiasi kikubwa na matumizi mabaya ya dawa.
Mganga Mfawidhi wa Zahanati ya Terrat, Tumaini Kamkama, anaeleza: “Ukitumia dawa kiholela, unaweza kuharibu ini, wengine wanaweza kupata madhara kwenye macho”
Wakazi wa vijijini mara nyingi hutegemea taarifa kutoka kwa marafiki, wauzaji wa maduka ya dawa au hata uzoefu wao wa zamani. “Ni ukiwa umechoka ama umemkosa daktari,” anasema mmoja.
Lakini dawa si chai Kuna wakati, kinachomezwa ni sumu ya polepole.
Kwa pamoja tunaweza kubadili hali hii. Elimu ya afya, ushauri sahihi, na huduma bora ndio suluhisho.
Je, dawa unazotumia ni tiba… au sumu?