
Katika juhudi za kupambana na ukatili wa kijinsia nchini Tanzania, ushiriki wa vijana umetajwa kuwa chachu muhimu ya mabadiliko chanya katika jamii. Katika kipindi cha Kurunzi Maalum cha Orkonerei FM Radio, wataalamu wa sheria na wanaharakati wa haki za binadamu wameeleza kuwa vijana wanapaswa kushirikishwa zaidi katika mijadala na maamuzi yanayohusu mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.
Kwa mujibu wa Takwimu za Demografia na Afya Tanzania (TDHS) za mwaka 2015/2016, asilimia 40 ya wanawake wenye umri wa miaka 15-49 wameripoti kufanyiwa ukatili wa kimwili, huku 17% wakiripoti kufanyiwa ukatili wa kingono. Hali hii inaonyesha ukubwa wa tatizo ambalo linahitaji juhudi za pamoja, hasa kwa kuwajumuisha vijana kama sehemu ya suluhisho.
Katika mahojiano maalum na Orkonerei FM Radio, Hassan Fussa, msaidizi wa kisheria kutoka Shirika la SELA, alifafanua maana ya ukatili wa kijinsia na namna unavyoweza kupunguzwa ikiwa vijana watapewa nafasi kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi yake.
Bi Honorata Raymond Nasua, Meneja Miradi kutoka Mtandao wa Mapambano Dhidi ya Ukatili wa Kijinsia (NAFGEM), alieleza kuwa ushirikishwaji wa vijana unaweza kusaidia kuibua suluhisho la kudumu kupitia elimu, mijadala na hatua madhubuti za kisheria. Alisisitiza kuwa mila na desturi zina nafasi kubwa katika malezi ya vijana, hivyo wazee wanapaswa kuwaelimisha watoto wao kwa kusimulia hadithi zenye mafunzo ya kupinga ukatili wa kijinsia.
Baadhi ya wanajamii waliozungumza na Orkonerei FM Radio walieleza kuwa viongozi wanapaswa kuwawezesha vijana kwa kuwapa elimu na nafasi za kushiriki katika maamuzi yanayohusu haki za kijinsia. Wakazi wa mkoa wa Manyara walisema kuwa ongezeko la matukio ya ukatili wa kijinsia linahitaji mbinu mpya, ikiwa ni pamoja na kuhamasisha jamii kupitia vijana wenyewe.
Katika kipindi hiki, pia ilipigwa nyimbo yenye ujumbe wa kupinga ukatili wa kijinsia kutoka Tanzania Police yenye jina “Ukatili wa Kijinsia, Mabadiliko Yanaanza na Mimi na Wewe”, ikisisitiza umuhimu wa kila mtu kuchukua hatua binafsi dhidi ya vitendo vya ukatili.
Kwa kuhitimisha, ushiriki wa vijana si tu unawapa uelewa wa athari za ukatili wa kijinsia bali pia unawafanya kuwa mabalozi wa mabadiliko katika jamii zao. Serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali na jamii kwa ujumla wanapaswa kushirikiana kuwajengea vijana uwezo wa kupambana na ukatili wa kijinsia kwa ujasiri na uthabiti.