
Nyangusi Ole Sang’ida
Ilkirevi, Arusha – Mwenyekiti wa Kijiji cha Ilkirevi kilichopo katika Kata ya Olturoto, Wilaya ya Arusha, Bw. Abraham Gerald Mollel ameongoza operesheni ya kijiji dhidi ya mbwa wakali waliowavamia na kuwadhuru binadamu pamoja na mifugo.
Katika tukio hilo la aina yake, mbwa zaidi ya 13 wameripotiwa kuvamia vitongoji vya Olturoto na Oloirowa, ambapo wamesababisha majeraha kwa mtoto mdogo wa miaka 4, kuua kuku takribani 30, na kondoo 6. Mzee mmoja alijeruhiwa kwa kung’atwa mguu. Msako uliohusisha vijana wa kijiji umefanikiwa kuwaua mbwa kati ya 6 hadi 8 hadi sasa.
Mwenyekiti Mollel amesema kuwa licha ya kutokuwa na sheria inayoruhusu moja kwa moja kuuawa kwa mbwa, hatua hiyo imelenga kulinda maisha ya binadamu na mifugo. Aidha, alisisitiza kuwa wamiliki wa mbwa waliowashambulia watu watafikishwa mahakamani.
“Fuga kwa starehe zako, lakini ukiwaachia wahatarishe watu, lazima utaitwa kujibu,” alisema Mollel.
Mkazi jirani Gidion Lengoisai alielezea tukio hilo kama la kutisha na kusema usiku huo alisikia kelele saa 8:25 usiku, na baada ya kufuatilia alikuta mbwa wakiua mifugo ya jirani. Juhudi za haraka za wananchi zilizuia madhara zaidi.
Mwenyekiti amesema msako bado unaendelea na ametoa wito kwa wamiliki wa mbwa kuwajibika ipasavyo ili kuepusha madhara kwa jamii.