
Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu imekabidhi pikipiki 16 kwa vikundi vitatu vya vijana kupitia mikopo ya asilimia 10, yenye thamani ya shilingi milioni 45.9. Lengo la mpango huu ni kuwawezesha vijana kujikwamua kiuchumi na kuimarisha ustawi wa jamii.
Akizungumza wakati wa makabidhiano mnamo Februari 13, 2025, Mkuu wa Wilaya ya Mbulu, Michael Semindu, aliwataka wanufaika kurejesha mikopo kwa wakati ili vijana wengine waweze kufaidika.
Mbunge wa Mbulu Vijijini, Mhe. Flatei Massay, amewahimiza vijana na wanawake kutumia fursa mbalimbali za kiuchumi zinazotolewa na serikali kwa maendeleo yao na jamii kwa ujumla.

Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, Joseph Mandoo, alisema kuwa mikopo hii ni sehemu ya juhudi za halmashauri kusaidia wananchi kupitia fedha za mapato ya ndani. Alibainisha kuwa halmashauri imekuwa ya kwanza kwa ukusanyaji wa mapato kwa miaka mitatu mfululizo, na fedha hizo zimewezesha utoaji wa mikopo yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 594, ambapo milioni 204 zimetolewa kwa awamu hii kwa vijana, wanawake, na watu wenye ulemavu.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mbulu, Abubakar Kuuli, alisisitiza kuwa mikopo ya asilimia 10 itaendelea kutolewa na kuwataka wanufaika kuhakikisha wanarudisha fedha hizo kwa wakati.
Vijana walionufaika na mkopo huo wameishukuru serikali kwa kuwapatia fursa ya mikopo isiyo na riba, wakisema itasaidia kuboresha maisha yao kiuchumi.
Katika hatua nyingine, halmashauri imekabidhi vitambulisho vya utambuzi kwa wajasiriamali 52 kwa awamu ya kwanza, ikiwa ni sehemu ya jitihada za kuwawezesha wafanyabiashara wadogo katika wilaya hiyo.