
Na Nyangusi ole Sang’ida
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika Viwanja vya Sheikh Amri Abeid ameongoza maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani ya mwaka 2025. Akiwahutubia wakazi wa Arusha na Watanzania kwa ujumla, Rais Samia ameeleza msimamo wake juu ya masuala muhimu katika ujenzi wa taifa, ikiwemo maboresho ya sera na sheria kuhusu umiliki wa ardhi kwa wanawake.
Aidha, Rais Samia amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha kila Mtanzania anakuwa na Bima ya Afya ili kupata huduma bora, hususan katika maeneo ya pembezoni. Amehimiza pia wazazi na walezi kote nchini kutenga muda na kuwasaidia watoto wao kukua katika mazingira salama, akisema kuwa malezi sahihi ndiyo chimbuko la kizazi chenye maadili na uwezo wa kuliletea taifa maendeleo.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Paul Makonda, amebainisha kuwa katika kipindi cha siku saba zilizopita kulikuwa na utekelezaji wa mambo makubwa manne, yakiwemo matukio ya kukuza uwezo wa wanawake, uhamasishaji wa umiliki wa ardhi, na kampeni za kuwajengea uelewa kuhusu haki na fursa zao.
Kwa upande wake, MamaHindu – mwakilishi wa moja ya mashirika yaliyoshiriki maadhimisho hayo – amesisitiza juu ya malezi bora kwa watoto wa Kitanzania, akisema ni jukumu la jamii nzima kuwajenga watoto katika misingi ya maadili. Ameongeza kuwa wanawake wanapaswa kupewa nafasi stahiki, ikiwemo haki ya kumiliki ardhi, ili kujenga uchumi imara kwa familia na jamii zote nchini.
Maadhimisho haya ya Siku ya Wanawake Duniani yameonyesha dhamira thabiti ya taifa katika kuimarisha usawa wa kijinsia na kuwajengea wanawake mazingira wezeshi katika kila sekta yakibebwa na kaulimbiu isemayo “Wanawake na Wasichana 2025: Tuimarishe Haki, Usawa na Uwezeshaji”.