

Na Nyangusi Ole Sang’ida
Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Arusha limetoa mafunzo maalumu kwa madereva wanaoendesha magari ya Serikali mkoani humo, ili kuwajengea uwezo wa matumizi sahihi ya barabara na mifumo mipya ya Jeshi hilo.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Arusha, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Zauda Mohamed, amesema mafunzo hayo ni mwendelezo wa mkakati wa Jeshi la Polisi wa kuyafikia makundi mbalimbali katika jamii ili kupunguza ajali za barabarani na kuongeza uelewa wa madereva kuhusu mifumo mipya ya Jeshi la Polisi kama mfumo wa ukaguzi wa magari, mfumo wa leseni na ukaguzi wa madeni ya Serikali.
Aidha, Kaimu Meneja wa OSHA Kanda ya Kaskazini, Bw. Abubakari Shabani, amesema madereva hao wamepewa pia elimu kuhusu umuhimu wa kupima afya ya macho mara kwa mara ili kupunguza ajali zinazosababishwa na matatizo ya kuona.
Kwa upande wake, Afisa wa Mazingira kutoka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Arusha, Bw. Gabriel, amesisitiza madereva kuzingatia alama zote za barabarani, hususan maeneo ya vivuko vya watembea kwa miguu, maegesho, na sehemu za kugeuzia magari ili kuepuka usumbufu na ajali.

Baadhi ya madereva waliopokea mafunzo hayo wameeleza kufurahishwa na elimu waliyoipata na kusema itawasaidia katika kuendesha magari yao kwa kuzingatia usalama wao na watumiaji wengine wa barabara.
Pia wametoa rai kwa madereva wenzao kuhakikisha wanajitokeza kwa wingi pindi wanaposikia uwepo wa mafunzo kama hayo, ili kuongeza ufanisi na usalama barabarani katika Mkoa wa Arusha na maeneo mengine nchini.