
Zaidi ya madereva 800 wa magari ya utalii mkoani Arusha wamepatiwa mafunzo maalumu yaliyoandaliwa na Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani, ikiwa ni maandalizi ya msimu wa utalii (high season) unaotarajiwa kuanza hivi karibuni.
Akifungua mafunzo hayo, Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) William Mkonda, amesema mafunzo hayo yamelenga kuwakumbusha madereva sheria, kanuni na matumizi sahihi ya barabara ili kuhakikisha usalama wa watalii unaimarishwa, na hivyo kuitangaza vyema Tanzania kama taifa salama.
Aidha, Mwenyekiti wa Chama cha Waendesha Watalii nchini (TTGA), Bw. Lembrisi Moses, amesema kuwa madereva hao wamejengewa uwezo mkubwa kupitia mafunzo hayo, huku akieleza kuwa wamekumbushwa umuhimu wa kuzingatia alama za barabarani na mwendo sahihi.
Naye mmoja wa madereva walioshiriki mafunzo hayo, Bw. Usia Israel, amesema kupitia elimu hiyo wamejifunza kuhusu udereva wa kujihami ambao utasaidia kupunguza ajali za barabarani ambazo zinaweza kuepukika.
Mafunzo haya ni sehemu ya mkakati wa Jeshi la Polisi katika kuwajengea uwezo madereva wa makundi mbalimbali ili kuhakikisha usalama unatawala kwenye sekta ya utalii nchini.